Wizara ya Maliasili na Utalii imeanza kufanya uchunguzi kwa
kushirikiana na mamlaka mbalimbali, ikiwemo Mamlaka ya Viwanja vya Ndege
(TAA) na vyombo vya ulinzi na usalama ili kubaini waliohusika na
upitishwaji wa nyara za serikali katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa
Julius Nyerere (JNIA) hivi karibuni.
Wizara hiyo pia imeeleza kupokea kwa masikitiko makubwa taarifa hizo
za kukamatwa kwa nyara za serikali katika Uwanja wa Ndege wa Zurich
nchini Uswisi zikiwa njiani kwenda China kutokea Uwanja huo wa Ndege wa
Kimataifa wa JNIA wa jijini Dar es Salaam.
Taarifa ya wizara hiyo kwa vyombo vya habari iliyosainiwa na Waziri Lazaro Nyalandu
ilisema wizara hiyo inaupongeza uongozi wa Uwanja wa Ndege wa Zurich na
Serikali ya Uswisi na watu wote walioshiriki kubaini na kukamata nyara
hizo.
Waziri Nyalandu alisema, nyara hizo zinajumuisha meno ya tembo yenye uzito wa kilo 262, kucha na meno ya simba vyenye uzito wa kilo moja.
Alisema tukio la kukamatwa kwa nyara hizo lilitokea kwenye uwanja huo
Julai 6, mwaka huu zikiwa ndani ya masanduku manane zikiwa njiani
kwenda Beijing China kutokea uwanja wa ndege wa Dar es Salaam kupitia
Zurich.
“Wizara imepokea kwa masikitiko
makubwa taarifa hizi na kwamba nyara hizo zimesafirishwa kupitia Uwanja
wa Ndege wa Julius Nyerere. Tukio hili linadhihirisha kuwa tatizo la
ujangili bado linaendelea ndani na nje ya nchi yetu” alisema.
Usikose kuangalia Movies mbalimbali kutoka kila kona ya dunia, bofya kwenye picha iliyopo hapo chini kuona izo muvies