Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa
(TAKUKURU) LINDI, imekanusha tuhuma za rushwa zilizoelezwa na baadhi ya
vyombo vya habari dhidi ya Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Halmashauri
Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (NEC-CCM), Nape Nnauye.
Kamanda wa Takukuru mkoani hapa, Steven Chami
alisema, taasisi hiyo haikumkamata Nape kwa sababu ya kuhusika na
rushwa, bali ilitaka kujiridhisha na kiwango cha fedha kilichokuwa
kikitolewa kwa mawakala.
Alisema, “Uhakiki
ulifanywa kwa watu wote walioomba ridhaa ya kugombea nafasi mbalimbali
mkoani humu, ikiwa ni pamoja na ubunge, ambao Nnauye na wengine
waliomba.”
Kutokana na maelezo yake, Nape alikuwa
miongoni mwa wanasiasa walioomba ridhaa ya CCM kugombea ubunge katika
jimbo la Mtama, na alikuwa pia miongoni mwa watangaza nia walioingia
kuchukua fedha katika Benki ya NMB ya mjini hapa, iliyotajwa na vyombo
vya habari.
Alifafanua kuwa, kitendo cha maofisa wa
Takukuru kumfuata Nnauye ili wajiridhishe na kiwango cha fedha
alichokitoa kwa ajili ya mawakala, kilichukuliwa kuwa ni kumkamata kwa
rushwa jambo ambalo si kweli.
“Vijana
wangu walimuomba Nnauye aongozane nao hadi ofisini ili wahakiki kiasi
cha fedha alichokuwa amekitoa benki. Alifanya hivyo na kutumia dakika
kati ya 30 na 45 kutoa maelezo yaliyowaridhisha maofisa wa Takukuru
waliomwachia baada ya mahojiano mafupi. “…Ninapenda kuwathibitishia
kuwa, Nnauye alikuwa na kiwango cha kawaida cha fedha ambacho
kinaruhusiwa kutolewa kwa mawakala. Haikuwa rushwa kama ilivyopotoshwa
na baadhi ya wanahabari walioandika na kutangaza habari hiyo,” Chami alisema na kuongeza kuwa alikutwa na Sh milioni tatu tu.
Alisema, Nnauye aliieleza Takukuru kuwa
fedha hizo zilikuwa kwa ajili ya kuwalipa mawakala wake 156, aliowaandaa
kusimamia uchaguzi katika vituo vyote jimboni humo.
Usikose kuangalia Movies mbalimbali kutoka kila kona ya dunia, bofya kwenye picha iliyopo hapo chini kuona izo muvies