Siku tatu baada ya Baraza Kuu la Chadema kuridhia kumpumzisha kwa muda Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa baada ya kutofautiana na Kamati Kuu kwa kumkaribisha waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa, kiongozi huyo amesema yupo salama na wakati mwafaka ukifika atazungumza ya moyoni.
Dk Slaa alisema amekuwa akisikia mengi yakisemwa juu yake lakini yote yamekuwa yakimchekesha tu. Hakuhudhuria vikao muhimu vya chama hicho na vile vya Ukawa,
vikiwamo; wakati Lowassa akitambulishwa rasmi, akichukua fomu, kikao cha
Baraza Kuu na juzi Mkutano Mkuu na hakuwa akipatikana kwa simu yake ya
mkononi.
Wakati kimya kikitawala juu ya hatima yake, baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikiandika kuwa amejivua uanachama Chadema.
Lakini jana alisema: “Naangalia
mambo mengi yanayoendelea kwenye mitandao halafu ninacheka tu,
usifikiri sifuatilii, nafuatilia kinachoendelea na ninabaki nikicheka.”
Kuhusu hatima yake kisiasa na madai ya kujiuzulu uanachama ndani ya
Chadema, alisema hawezi kuzungumza lolote kwa sasa na atafanya hivyo
wakati mwafaka ukifika. “Usijali wakati wangu wa kuzungumza ukifika nitasema tu, sasa hivi nawaachia mzungumze, lakini nitazungumza,” alisema.
Kadhalika, alipoulizwa kuhusu taarifa zilizozagaa kuwa maisha yake
yapo hatarini kwa kuwa anatishwa, Dk Slaa alisema hata hilo pia
atalizungumzia wakati mwafaka ukifika.
“Ndiyo hayohayo ninayosema, wala msijali nitazungumza wakati ukifika,” alisema na kusisitiza: “Nipo salama.”
Dk Slaa alisema kwa sasa yupo mapumzikoni nje ya jiji la Dar es Salaam ingawa hakutaka kueleza ni eneo gani. Juzi, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alifafanua tofauti iliyojitokeza kati ya Kamati Kuu ya Chadema na Dk Slaa wakati wa mchakato wa kumpokea Lowassa.
Katika mkutano huo wa Baraza Kuu la Chadema, Mbowe alisema wamekubaliana katibu mkuu huyo apumzike kwa muda...
“Nina hakika kwa tabia na hulka za Dk Slaa… kwa sababu anajua
tunampenda na yeye anakipenda chama hiki, tunamwombea kwa Mungu ampe
nguvu na ujasiri wa kuona kwamba kauli ya wengi ni kauli ya Mungu.”
Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo na makada wengine wa
Chadema, jana walikwenda kuonana na Dk Slaa nyumbani kwake na kufanya
naye kikao cha faragha.
Picha zilizomuonyesha Ndesamburo akiwa na Dk Slaa na makada wengine akiwamo Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Jaffar Michael, zilisambaa kwa kasi katika mitandao ya kijamii jana na kuibua mijadala.
Usikose kuangalia Movies mbalimbali kutoka kila kona ya dunia, bofya kwenye picha iliyopo hapo chini kuona izo muvies