Dodoma. Bunge Maalumu la Katiba leo linaanza wiki ngumu pale litakapohitimisha mjadala wa muundo wa Muungano na kupiga kura kupitisha au kukataa.

Ili zipite, ni lazima zipate theluthi mbili ya kura kwa kila upande wa Muungano.Hata hivyo, leo Bunge hilo litaanza kwa kumpa nafasi Mjumbe wa Bunge hilo, Tundu Lissu kuendelea kutoa ufafanuzi wa hoja za walio wachache kwenye Kamati Namba Nne.
Ufafanuzi huo wa Lissu uliahirishwa juzi baada ya matangazo ya moja kwa moja ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kukatika ghafla. Baada ya Lissu kumaliza, kamati zilizobaki ambazo ni Namba Sita inayoongozwa na Steven Wassira, Kamati Namba Saba inayoongozwa na Brigedia Jenerali mstaafu Hassan Ngwilizi zitawasilisha taarifa zao.
Inatarajiwa kuwa katika kipindi cha mchana, Kamati Namba 10 inayoongozwa na Anna Abdallah itawasilisha taarifa yake na kufuatiwa na ufafanuzi wa wajumbe walio wachache wa kamati hizo.
Kulingana na hali ya mambo ilivyo, kuna uwezekano mkubwa kwamba wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, wataanza kuchangia taarifa za kamati zote 12 katika kipindi cha jioni au kesho asubuhi.
Kwa mujibu wa Kanuni ya 33 (7), baada ya taarifa ya kamati hizo kuwasilishwa, zitajadiliwa katika kipindi kisichozidi siku tatu. Kama mambo yatakwenda kama ilivyo, inatarajiwa kuwa upigaji wa kura kupitisha sura hizo mbili huenda ukafanyika Ijumaa na hivyo kutegua kitendawili cha muda mrefu kuhusu aina ya muundo wa Muungano katika Katiba Mpya.