Mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk John Magufuli,
na mgombea mwenza, Samia Suluhu Hassan jana walichukua fomu kutoka Tume
ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), huku Rais Jakaya Kikwete akisema wapinzani
wataisoma namba.
Ofisi ndogo za makao makuu ya CCM
zilizoko Lumumba na za Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), zilifurika
mashabiki waliovalia nguo za rangi ya njano na kijani, ambazo hutumiwa
na chama hicho, huku wakazi wengine wanaofanya kazi au kuishi maeneo
jirani na barabara za Morogoro, Bibi Titi na Ohio, wakilazimika
kusimamisha shughuli zao kwa muda kushuhudia msafara wa wagombea hao
ukipita.
Walinzi wa ofisi za NEC walilazimika
kufanya kazi ya ziada kudhibiti wafuasi wa CCM waliosindikiza wagombea
hao kutoka ofisi ndogo za CCM kabla ya msafara huo kuondoka baada ya
wawili hao kuchukua fomu, kurejea Lumumba, ambako mwenyekiti wa chama
hicho, Rais Jakaya Kikwete aliupokea.
“Wakwere wanasema chihendo na mwene mwana, yaani shughuli na mwenye mtoto,”
alisema Rais Kikwete mara baada ya msafara kuwasili akieleza sababu za
yeye kuwapo eneo hilo kwa kutumia maneno ya shughuli za kitamaduni za
jandoni, unyagoni na mkoleni za kabila la Wakwere.
“Nimekuja
hapa kujiridhisha kama kweli fomu zimechukuliwa. Na kweli nimeziona.
Baada ya hatua hii wale wanaodhani kuwa CCM ni chama cha mchezo mchezo,
wataisoma namba.”
Huku akikatiza hotuba yake kwa kuitaka bendi ya TOT ya chama hicho kuimba wimbo wa “Shangilia Ushindi Unakuja”, Rais Kikwete alisema kwa kuwa yeye ni baba alilazimika kuja kuangalia kama mwanaye ametekeleza alichotuma.
Kikwete, ambaye alitumia mifano
iliyovunja mbavu wafuasi hao, alirusha kijembe kwa wanachama walioihama
CCM akisema ni tamaa na kuahidi kufanya mkutano mkubwa wa uzinduzi wa
kampeni.
“CCM
shangilia ushindi unakuja, tena ushindi wa uhakika na si wa wasiwasi.
Baada ya hapa kitakachofuata ni uzinduzi hapo Agosti 22 kwenye mkutano
utakaotisha. Hatumwi mtoto siku hiyo, unakuja mwenyewe,” alisema.
“Watu wanasumbuliwa na tamaa na wakati mwingine ni tamaa iliyopitiliza kutaka madaraka.”
Magufuli alitoka ofisi ya CCM Lumumba
akiwa amepanda gari aina ya Toyota Land Cruiser iliyokuwa wazi juu akiwa
na msafara wa magari yapatayo 10 kuelekea ofisi za NEC. Baada ya kufika
eneo la makutano ya Barabara ya Ohio na Bibi Titi, alishuka na kupanda
gari nyingine iliyokuwa wazi nyuma na kuamsha kelele za shangwe.
Aliwasili ofisi hizo saa 5.22 asubuhi na
baada ya kuchukua fomu za kuwania urais, msafara wa kurejea ofisi za
chama hicho zilizoko Lumumba ulianza tena na kufika ofisi hizo ndogo za
CCM, ambako ulipokelewa na Rais Kikwete.
“Matatizo ya Watanzania nayajua na
ninaahidi kuwa nitakuwa mtumishi wenu mtiifu,” alisema Dk Magufuli
baada ya Rais Kikwete kumuomba aketi ili azungumze na wafuasi wa chama
hicho.
“Nafahamu kuwa Watanzania wanahitaji
ajira na hawataki usumbufu kwenye biashara zao kama mamantilie, wana
kero kwenye huduma mbalimbali. Ninawaahidi kuwa nitazishughulikia.
“Napenda
nimhakikishie mwenyekiti na wananchi mliokusanyika hapa kuwa CCM
itashinda na wala simuoni mtu wa kutushinda. Nashukuru kwa moyo
mliouonyesha wa kunisindikiza mimi pamoja na Samia. Mmetoa jasho na
mmepoteza muda wenu. Napenda kuwahakikishia kuwa muda wenu hautapotea
bure.”
Alirudia wito wake wa kuwataka wananchi
kuendeleza mshikamano uliopo bila kujali itikadi zao wala makabila ili
kuliletea Taifa maendeleo kwa kuondoa kero zinazowakabili.