MWANANCHI
Baada ya vuta vikuvute ya muda mrefu, hatimaye leo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kinatarajia kumtangaza mgombea wake wa urais katika mkutano maalumu utakaofanyika jijini Mwanza.
Habari zilizopatikana na kuthibitishwa
na viongozi wa chama hicho Kanda ya Ziwa Magharibi na makao makuu
zilisema kuwa leo mgombea huyo atatangazwa mkoani hapa huku zikibainisha
kuwa anayepewa nafasi kubwa ni Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa.
Taarifa hizo zimekuja wakati kukiwa na tetesi kuwa chama hicho kilikuwa kinafanya mazungumzo na waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa
aliyekuwa anawania urais kupitia CCM na kutemwa katika hatua za awali,
huku vyanzo mbalimbali vikisema mazungumzo hayo yanachukua muda mrefu na
kuna uwezekano mkubwa wa kutozaa matunda.
Jana, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe
pamoja na baadhi ya wabunge walikaririwa wakitoa matamko ya
kumkaribisha Lowassa kuingia Chadema lakini kwa sharti la kufuata kanuni
na taratibu za chama hicho, lakini Dk Slaa alisita kumzungumzia
kiongozi huyo akiahidi kuzungumza mambo yatakapokuwa sawa.
Mratibu wa Operesheni za Chadema Kanda ya Ziwa Magharibi, Tungaraza Njugu
alisema mgombea huyo (bila kumtaja jina), atatangazwa katika mkutano wa
hadhara utakaofanyika kwenye Viwanja vya Magomeni, Ilemela kuanzia saa
nane mchana.
Njugu alisema katika mkutano huo, viongozi wakuu wa Ukawa wanatarajia kuwapo na maandalizi yake yamekamilika.
“Kesho
(leo) tutakuwa na mkutano mkubwa kwenye viwanja vya Magomeni,” alisema
Njugu na kuongeza: “Mgombea urais kupitia Ukawa atajulikana hapo, kwani
tunatarajia viongozi wakuu wa Ukawa watamtangaza.”
Katika mazingira tofauti, akihutubia mkutano wa hadhara mjini Geita juzi, Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu
alidokeza jina la Dk Slaa kama mgombea urais wa chama hicho, kitendo
kilichoibua hamasa na umati kumshangilia, lakini akawapoza akisema ulimi
umeteleza.
Alipoulizwa kuhusu mkutano huo, Mwenyekiti wa NLD, Dk Emmanuel Makaidi
alikiri kuwa leo kulikuwa na mpango wa kumtangaza mgombea wa Ukawa,
lakini alidhani ingekuwa Dar es Salaam, hivyo kwa kuwa wameamua iwe
Mwanza angefanya utaratibu wa ndege ili aweze kuwahi.
Mwenyekiti wa NCCR- Mageuzi, James Mbatia hakupatikana kuzungumzia mkutano huo, lakini Katibu Mkuu wa chama hicho, Mosena Nyambabe
alisema hakuwa na taarifa hizo, hasa kwa kuwa vikao vya mwisho
vilivyofanyika Jumapili na Jumatatu vilihusisha wenyeviti wa vyama
pekee.
Hata hivyo, alisema ilibidi mgombea huyo
atangazwe ama jana au leo. Chama cha CUF kimekwishatangaza kuwa
kinasubiri uamuzi wa kikao cha Baraza Kuu la Uongozi litakaloketi Julai
25 kuamua juu ya hatima yake ndani ya Ukawa.
Alipotakiwa kudokeza ni nani atasimama
kuwakilisha Ukawa, Njugu alisema jukumu hilo ni la viongozi wa juu na
kwamba yeye akiwa kiongozi wa Kanda anatambua mgombea urais wa Ukawa
atatangaziwa Mwanza leo.
MTANZANIA
Vituko vimeanza katika kampeni za kuwania kuteuliwa na CCM kugombea nafasi za Ubunge katika majimbo mbalimbali nchini.
Moja ya vituko hivyo ni kile kilichotolewa na Mbunge wa Dodoma Mjini anayemaliza muda wake Dk.David Mallole
ambaye jana wakati akijinadi kwa wanachamawa chama hicho, aliwaomba
wamteuwe kwa mara nyingine kwa sababu amesoma darasa moja na mgombea
Urais John Magufuli.
Wakati hayo yakijiri Dodoma, Jimbo la Kinondoni msanii Steve Nyerere aliomba achaguliwe kwani ana uwezo wa kupita katika ofisi za mabalozi wa nje waliopo jijini Dar es salaam kuomba misaada.
Kampeni hizo zilianza jana wakati Dar
wakati wagombea wakijinadi mbele ya wajumbe kabla ya kupiga kura ya
maoni Agosti mosi mwaka huu.
“Wilaya
ya Kinondoni ndio inayoongoza kwa kuwa na ofisi nyingi za mabalozi,
mkinichagua nitahakikisha nakwenda wenye Ubalozi wa Marekani kuomba
misaada kwa ajili ya kuwawezesha vijana…Nitakwenda Ubalozi wa China
kuomba atusaidie kuondoa mafuriko yanayolijumba jimbo hili “Steve Nyerere.
Katibu wa CCM,Kinindoni alisema katika
Wilaya yake kuna wagombea 60 ambao kati yao wanawake wanne wanawania
majimbo ya Kinondoni,Kawe, Ubungo na Kibamba.
NIPASHE
Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Mkoa wa Dodoma, Mariam Mfaki, alifariki dunia jana katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.
Mtoto wa marehemu, Mohamed Mfaki, alisema mama yake alifariki majira ya saa sita mchana.
Alisema mama yake mpaka kufikwa na mauti hayo alikuwa anasumbuliwa na saratani ya utumbo.
“Alianza
kuugua tangu mwaka 2012 vidonda vya tumbo, baadaye utumbo ulipata
tatizo lililosababisha saratani ya mapafu na utumbo, baada ya kuendelea
na matibabu hayo akapata pia ugonjwa wa moyo,” alisema.
Mohamed alisema marehemu alianza
kutibiwa katika Hospitali ya Apollo nchini India mwaka 2012 mpaka mwaka
2014 huku akiwa anaendelea na shughuli zake ikiwamo kuhudhuria vikao vya
Bunge.
“Marehemu
alizidiwa usiku wa Julai 19 mwaka huu na kupelekwa katika Hospitali ya
Rufaa ya Mkoa wa Dodoma kwa ajili ya matibabu, ilipofika jana majira ya
saa tano asubuhi hali ilibadilika hatimaye saa sita mchana akaaga
dunia,” alisema.
Alisema taratibu za mazishi zinaendelea
na kwamba wao kama familia wamepanga mazishi yafanyike leo saa 10 jioni
shambani kwake maeneo ya Miyuji, Manispaa ya Dodoma.
Alipoulizwa kama ofisi ya Bunge ina
taarifa za msiba huo, alisema taarifa wanazo na tayari baadhi ya maofisa
walifika nyumbani kwa marehemu Area E.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Ezekiel Mpuya, alithibitisha kutokea kifo hicho na kwamba kilitokea majira ya saa tano asubuhi.
Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashillilah, alipotafutwa kwa njia ya simu kuelezea kifo hicho cha Mbunge, simu yake haikupokelewa.
Marehemu alikuwa Mbunge wa Viti Maalum kwa vipindi vitatu kuanzia mwaka 2000 hadi Bunge lilipovunjwa Julai 9, mwaka huu.
Kabla ya kuwa mbunge, alikuwa Afisa
Tarafa kwa zaidi ya miaka 20 katika wilaya mbalimbali za Mkoa wa Dodoma.
Ameacha mume, watoto sita na wajukuu 10.
NIPASHE
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), leo inatarajia kuanza uandikishaji wananchi katika Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa mfumo wa Teknolojia ya Biometric Voters Registration (BVR) katika Jiji la Dar es Salaam, huku kukiwa na wasiwasi mkubwa kuhusu idadi ya mashine zitakazotumika kwa kila kituo.
Hadi jana majira ya mchana, baadhi ya
ofisi za kata za Manispaa za Temeke, Ilala za jiji hilo zilikuwa bado
hazijapelekewa mashine hizo, isipokuwa Ubungo, katika Manispaa ya
Kinondoni ilikuwa na takriban BVR 14.
Manispaa ilieleza kuwa kila kituo
kitakuwa na BVR moja, tofauti na maelezo ya awali yaliyotolewa na Nec,
kwamba kila kimoja kingekuwa na mashine mbili.
Katika Ofisi za Manispaa ya Kinondoni,
pilikapilika za watu, wakiwamo maofisa watendaji wa Kata, waliofika
katika ofisi hizo kufuata mashine hizo.
Ofisa Uchaguzi wa Manispaa hiyo, Valence Urassa, alisema mashine 706 zilikuwa zimepokelewa katika ofisi hizo hadi majira ya jioni.
Kwa mujibu wa Valence, manispaa hiyo ina vituo vya kuandikishia wananchi 706 na kila kituo kimoja kitakuwa na BVR moja.
Ofisa Mwandikishaji Msaidizi wa Manispaa ya Temeke, Waziri Kombo,
alisema BVR zote 572 zilikuwa zimepokelewa kwa ajili ya kusambazwa leo
asubuhi kwenye vituo 572 na kwamba kila kituo kitakabidhiwa mashine
moja.
Ofisa Uchaguzi wa Manispaa ya Ilala, Baina Hilary,
alisema mashine zilizopelekwa katika ofisi yao zilikuwa 396 ambazo ni
sawa na idadi ya vituo vya kuandikishia wananchi katika daftari hilo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Nec, Julius Malaba,
alisema mashine zilizoagizwa kwa ajili ya uandikishaji nchi nzima zipo
8, 000 na zinazotarajiwa kutumiwa kwa Dar es Salaam ni zaidi ya 3,000.
Usikose kuangalia Movies mbalimbali kutoka kila kona ya dunia, bofya kwenye picha iliyopo hapo chini kuona izo muvies