MWANANCHI
Mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Mosha Mahona
ameuawa na wananchi baada ya kuwachoma kwa kisu abiria watano waliokuwa
kwenye daladala linalofanya safari zake kati ya Posta na Ubungo Simu
2000. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura
alisema jana kuwa tukio hilo lilitokea juzi saa moja usiku katika eneo
la Magomeni Usalama na Mahona aliuawa kwa kushambuliwa na wananchi baada
ya kudhuru abiria wenzake.
Kamanda Wambura alisema Mahona alikuwa
ndani ya daladala hilo lililokuwa likitokea Posta kwenda Kituo cha Simu
2000 ndipo alipotoa kisu hicho na kuwashambulia wenzake sehemu
mbalimbali ya miili yao.
“Mahona
aliuawa na wananchi baada ya kuwachoma kwa visu abiria watano ambao
walipelekwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu.
Majeruhi hao wanaendelea vizuri,” Wambura.
Wambura alisema baada ya Mahona kufanya kitendo hicho walianza kumshambulia na kusababisha kifo chake.Aliwataja abiria waliochomwa visu kuwa ni; Daudi Mwenera, Geogre Nomani, Bakari Andrew, Zawadi Mwaipopo na Eda Kiwege.
Alisema polisi wanaendelea na uchunguzi
ili kujua sababu ya marehemu huyo kufanya kitendo hicho na mwili wa
marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Muhimbili kwa uchunguzi zaidi.Hilo ni tukio la kwanza la aina yake kwa abiria kuchoma visu wenzake.
MWANANCHI
Mbunge wa Viti Maalum alihama juzi CCM na kujiunga Chadema, Ester Bulaya
amesema licha ya kuahidiwa vyeo vingi ukiwamo uwaziri na ukuu wa wilaya
ili asihame CCM, aliamua kuviacha ili aweze kuwasaidia Watanzania wa
chini ambao wameonewa na serikali ya chama hicho kwa miaka 50 iliyopita.
Akihutubia katika mkutano wa hadhara
uliofanyikia katika Viwanja vya Stendi ya zamani mjini Bunda jana,
Bulaya alisema wakati chama chake cha zamani kilipogundua mikakati yake
ya kuhamia Chadema, makada wake walimwendea wakimsihi asitoke, bali
abakie ili apatiwe ukuu wa wilaya au uwaziri.
Bulaya aliyeambatana na Mbunge wa Kahama, James Lembeli
ambaye pia alijiunga na Chadema juzi, alisema baada ya kutafakari kwa
muda mrefu uhalisia wa maisha ya Watanzania hasa wa vijijini na jinsi
ambavyo Serikali ya CCM imekuwa ikiwatendea, aliamua kuachana na ahadi
hizo na kujiunga na Chadema kwa kuwa inalenga kuwakomboa Watanzania.
“Ngojeni
niwaambie, niliahidiwa ukuu wa wilaya na uwaziri ilimradi tu nisihame
CCM. Lakini nikaona yote hayo ni upuuzi, bali cha muhimu ni kuwakomboa
Watanzania, nikaachana nayo yote nikaja Chadema,” alisema.
Bulaya aliyejigamba kukulia na kufanya
kazi ndani ya CCM, alisema chama hicho hakina sera zozote za kuwakomboa
Watanzania badala yake kuna za kuwanufaisha wachache, jambo ambali yeye
na Lembeli hawakulitaka.
Bulaya alitangaza azma yake ya kugombea
ubunge katika Jimbo la Bunda Mjini, akisema tayari ameshajaza fomu za
kuomba kuteuliwa na chama hicho kugombea nafasi hiyo.
“Niwaambie
tu kwamba nimeshajaza fomu na kuirejesha na kesho (leo) nitashiriki
kura za maoni. Inshallaah Mungu akinisimamisha nitagombea nafasi hiyo na
nina uhakika wa kushinda,” Bulaya.
Lembeli aliwataka wakazi wa jimbo hilo
kutoipigia kura CCM katika Uchaguzi Mkuu ujao, badala yake waichague
Chadema kwa nafasi zote bila kumsahau Bulaya kwa ubunge kwa kuwa ni mtu
mwadilifu.
Mwenyekiti wa Bawacha, Halima Mdee
akihutubia mkutano huo aliwataka Watanzania wakubali kula fedha
wanazogawa na makada wa CCM ili wachaguliwe kwa nafasi mbalimbali za
urais, ubunge na udiwani lakini kura zote waipatie Chadema.
MWANANCHI
Uchaguzi wa kura za maoni ndani ya
Chadema katika Jimbo la Bariadi umeahirishwa baada ya kubainika kwa
matukio yanayoashiria vitendo vya rushwa.
Wakizungumza baada ya kuahirishwa kwa
uchaguzi huo, wajumbe wa mkutano mkuu wa wilaya walisema hawataki
kuingiliwa na virusi vya rushwa ndani ya chama hicho, kwa kuwa hali hiyo
italeta mpasuko na makundi.
Wajumbe hao wameutaka uongozi Chadema
kuwa makini na wanachama mamluki wanaohama kutoka vyama vingine vya
upinzani ili wasikivuruge.
“Hatua
ya kuahirishwa kwa uchaguzi inaonyesha ni namna gani chama kilivyo
makini ili wanaotoa rushwa wajifunze umakini huu na wananchi waelewe
kuwa chama kinatetea wanyonge,” Makula Saguda.
Hata hivyo, mjumbe mwingine, Masanja Lujani
alipinga hatua hiyo akisema kuahirishwa uchaguzi ni ubadhilifu ambao
haufai akisisitiza kuwa kama wamekamata mtu akiwa anagawa rushwa
wangemtoa katika uchaguzi na wengine wakaendelea.
Msimamizi wa uchaguzi huo, Emmanuel Mbise alisema uchaguzi huo umeahirishwa baada ya kukamata watu wakigawa rushwa kwa baadhi ya wagombea.
“Chadema
kinaaminiwa na kinapendwa na watu kwa sababu hakikubaliani na rushwa,
kwa mujibu wa katiba na mamlaka niliyopewa, nimeamua kuahirisha uchaguzi
hadi utakapotangazwa tena kutokana na uchaguzi huu kutawaliwa na
rushwa,” Mbise.
Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Simiyu, Wilson Mshuda ambaye pia ni mgombea katika jimbo hilo alisema: “Hatuwezi
kunyamaza kimya, hata katiba ya chama kuanzia ukurasa wa 86 inaongelea
mgombea ambaye ataonekana kutoa rushwa kwa wajumbe kuwa atakuwa
amejiondoa katika kinyang’anyiro.”
Jimbo la Bariadi lina wagombea 12 ambao ni Godwin
Simba, Mshuda, Masanja Madoshi, Seni Silanga, Manyangu Kulemwa,
Zacharia Shigukulu, Maendeleo Makoye, Sweya Makungu, Sitta Mulomo,
Wilson Limbu, Slivatus Masanja na Ntemi Ndamo.
Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo amesema pamoja na kuwa hatagombea nafasi hiyo, CCM isitarajie kulikomboa jimbo hilo.
MWANANCHI
Wakati uandikishaji wa wananchi katika
Daftari la Kudumu la Wapigakura, ukiingia siku ya tatu leo, kasoro
lukuki zimeendelea kugubika mchakato huo huku katika baadhi ya vituo
wananchi wakizichapa wakigombania kuingia chumba cha kujiandikisha.
Tukio la kutwangana makonde lilitokea
katika Kituo cha Shule ya Mwangaza, Gongo la Mboto saa 2.15 asubuhi
wakati uandikishaji ulipokuwa ukianza.
Mashuhuda wa tukio hilo walisema:
“Polisi unaowaona wamefika muda si mrefu, wala hawakuwepo hapa tangu
asubuhi… ninadhani walipewa taarifa baada ya watu kuanza fujo
wakigombania kuingia ndani kujiandikisha,” alisema Magreth John na kuongeza:
“Watu
wamepigana kwa sababu wanasema kuna wenzao ambao majina yao
hayakuandikwa jana (juzi) halafu wamefika asubuhi wakaanza kuitwa ndani
kujiandikisha. Hapo ndipo mzozo ulipoanzisha na ngumi zikafumuka.”
Msimamizi wa kituo hicho, Ramadhani Mshindo alisema mzozo huo ulitokea kwa sababu ya wananchi hao hawakuelewa utaratibu.
“Jana
(juzi) jioni wakati tunafunga zoezi hili saa 12.00 jioni kuna watu
wengi walikuwa kwenye foleni ambao hawakuandikishwa, kwa hiyo
tuliwaandika majina ili leo (jana) wakifika hapa watangulie kuandikishwa
kabla ya wengine. Sasa tulivyofika na kuanza kuita majina yao ili
waingie kujiandikisha ndipo watu wakaanza fujo na kupigana ikabidi
tupige simu polisi ili waje kutuliza ghasia,” alisema Mshindo.
Katika Kituo cha Shule ya Msingi Jica,
Tabata wananchi walilalamikia suala la muda kwani waandikishaji
walichelewa na hadi saa 4.30 asubuhi, asilimia kubwa ya watu hawakuwa
wamepata huduma. “Nimefika hapa
saa 12.00 asubuhi lakini hadi sasa sioni dalili ya kuandikishwa leo…
Wametuambia wanaanza kuandikisha wale waliobaki jana kwa sababu majina
yao yaliandikwa kwa hiyo sisi wa leo tunasubiri kwanza,” alisema Maria Saleh.
Maria alisema uandikishaji unakwenda taratibu kutoka na mashine kugoma mara kwa mara.
Malalamiko kama hayo yalitolewa na
wananchi waliokuwa wamefika kujiandikisha katika Kituo cha Shule ya
Msingi, Ulongoni, Gongo la Mboto na waandishi wetu walishuhudia watu
wengi wakiwa kwenye misururu, wengine wakiwa wamelala pembeni ya kituo
hicho baada ya kuchoka kusimama muda mrefu.
Hata hivyo, kwenye kituo hicho, wananchi
walijiwekea utaratibu kwamba kila mtu anayefika anaandika namba kwenye
daftari na kupewa kikaratasi kidogo chenye namba hiyo ndipo anapanga
foleni.
Utaratibu ambao ulisaidia kupunguza usumbufu na kuondoa vuta ni kuvute wakati wa kuingia kwenye chumba cha kujiandikisha.
Lakini licha ya kujiweka utaratibu huo, Ibrahim Kitumbi alisema changamoto ya muda na vifaa ilikuwa palepale.
“Hivi
tunavyozungumza watu waliyopewa namba wamefika 2,145. Hawa wameandika
majina tu na kupewa namba. Waliojiandikisha tangu jana hawafiki hata
200. Sasa kwa siku nane zilizobaki kweli tunaweza kumaliza kuandikishwa!
Huku si kutunyima haki?” alihoji.
Wakati wananchi wakitoa malalamiko hayo,
Ofisa Mtendaji wa Mtaa wa Ulongoni, Majura Mtalemwa alisema zoezi la
uandikishaji linakwenda vizuri tofauti na wananchi wanavyolilalamikia.
Mkazi wa Temeke, Steven Almasi aliyefika
kujiandikisha katika Kituo cha Magogoni, Yombo alisema mwaka huu wa
uchaguzi kuna uwezekano mkubwa wa baadhi ya wananchi kutoshiriki
uchaguzi.
Mtendaji wa mtaa huo, Zeddy Zeddy alikiri kuwapo baadhi changamoto kwenye kituo chake ikiwamo uchache wa mashine za kuandikisha.
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Julius Malaba
alisema wakazi wote wa jiji hili waliojitokeza wataandikishwa hata
baada ya siku zilizopangwa kumalizika hivyo hawatakiwi kuwa na hofu.
HABARILEO
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki ameomba mashine za kuandikisha wapigakura kwa mfumo wa kielektroniki (BVR), ziongezwe katika vituo vyenye matatizo ya mashine hizo na vyenye idadi kubwa ya watu.
Pia, ametaka mafundi wanaoshughulikia ukarabati wa mashine hizo, kuwa karibu na vituo muda wote ili kutatua changamoto hizo.
Amewataka wakazi wa mkoa huo kuwa
wavumilivu, kutokana na changamoto kadhaa zilizojitokeza siku ya kwanza
ya uandikishaji katika mfumo wa BVR.
Amesisitiza kuwa changamoto hizo, zinaendelea kutatuliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).
Alisema hayo jana baada ya kutembelea
vituo katika wilaya zote tatu za Dar es Salaam. Alikiri kukumbana na
changamoto kadhaa katika uandikishaji, ikiwa ni pamoja na maeneo mengi
mashine za BVR kuelemewa na kushindwa kufanya kazi.
Alisema kwa kawaida mashine hizo,
zinatakiwa kuandikisha watu 100 hadi 200, lakini baadhi ya maeneo
wanaishia kuandikisha watu 70, kutokana na mashine hizo kuchoka baada ya
kufanya kazi mikoani.
Hata hivyo, aliwahakikishia wananchi
wote kuwa wataandikishwa na hakuna mtu atakayeachwa. Katika wilaya ya
Kinondoni, hali imeendelea vizuri huku changamoto kubwa ikionekana kuwa
ni mashine za BVR kusumbua mara kwa mara, jambo linalosababisha
kuhudumia watu wachache kwa muda mrefu.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati
tofauti katika vituo tofauti vya wilaya hiyo, wananchi walisema hakuna
shida yoyote wanayoipata, isipokuwa kulazimika kukaa muda mrefu vituoni,
ambapo katika vituo hivyo mpaka kufikia mchana walikuwa wameandikisha
kati ya watu 30 hadi 70.
“Foleni
ni kubwa kweli lakini watu wengi hawapo, wakifika wanachukua namba na
kuondoka, hakuna tatizo lolote isipokuwa hizi mashine mara kwa mara
zinagoma na muda unakwenda,” alisema mkazi wa kata ya Ali Maua A, Mohammed Mavula.
Mkazi huyo wa Kijitonyama, akiwa katika
kituo cha Serikali ya Mtaa Kijitonyama alisema tangu alipofika katika
kituo hicho, hali iko shwari hakukua na tatizo zaidi ya uandikishaji
kwenda taratibu, na hivyo kushauri Serikali iongeze na siku za
kujiandikisha, akijenga hoja kuwa, Dar es Salaam ina wakazi wengi
ikilinganishwa na mikoa mingine nchini.
Hali ya vituo vingi Kinondoni,
ilionekana kuwa ni shwari na watu waliokaa kwa utulivu walioridhika kwa
utaratibu uliokuwa ukitumika wa aidha kupewa namba na kusubiri huku
wengine wakiondoka na kurudi baadaye au kuandikishwa majina yao kwa watu
hamsini hamsini au mia moja.
Vituo hivyo havikuwa na watu wengi sana
na pia hakukua na misururu ya kutisha kutokana na utaratibu huo kusaidia
kupunguza watu kurundikana katika vituo vya kujiandikishia. Hata hivyo
kutokana na vituo vingi jana kuandikisha watu wachache kutokana na
kusumbua kwa mashine na vifaa kuchelewa kufika vituoni katika baadhi ya
vituo, waliokwama juzi ndio walioanza kuhudumiwa.
“Baadhi ya watu wanaamua kuondoka tu kwa
sababu wakifika na kukuta namba zimefika mpaka 300 wanakata tamaa na
kuondoka zao,” alisema mkazi wa kata ya Kijitonyama Husna Juma.
Ofisa wa Uandikishaji, Farida Kimbanga
alisema uandikishaji unakwenda vizuri hata hivyo changamoto za hapa na
pale zinaweza kujitokeza, ambazo ni za kawaida na wanazitafutia ufumbuzi
mara moja na kwamba hakuna vurugu zozote ambazo zimejitokeza.
Ilala waongezeka Hali kama hiyo
ilielezwa kutoka katika Manispaa ya Ilala, ambako hali ilikuwa shwari na
idadi ya watu ikizidi kuongezeka. Kwa sehemu kubwa, changamoto ilikuwa
katika mashine, kwani uandikishaji ulikuwa wa taratibu. Mathalani,
kufikia saa nane baadhi ya vituo viliandikisha watu wasiozidi 50 kuanzia
asubuhi.
Katika vituo vilivyoandikisha watu
wachache ni vile ambavyo mashine za uandikishaji zilisumbua ikiwemo
kutoa picha zinazojirudia. Wakala wa Tume ya Uchaguzi (NEC) katika kituo
cha kujiandikisha cha mkoani kilichopo Ilala, Steve Johnson alisema
mashine hizo zilifanya kazi asubuhi na baadaye kuanza kutoa picha
zinazojirudia hivyo kusitisha uandikishaji kwa mashine moja.
Alisema katika kituo hicho kuna mashine
tatu za uandikishaji hivyo kubaki mbili ambazo mpaka mchana
ziliandikisha watu 40 huku kwa siku ya jana waliandikisha watu 68 katika
kituo hicho.
Nako katika kituo kwa Mtendaji Kata wa
Ilala, mpaka mchana walikuwa wameandikisha watu 150 ambao wanakaa mstari
kwenye mafungu ya watu kumi kwenye mashine nne zilizopo ukiacha
wanawake wajawazito na wenye watoto ambao hawapangi mstari.
Imeelezwa kuwa kwa siku ya jana, hali
ilikuwa nzuri kwa uandikishaji kwenda haraka haraka kwani wasimamizi
wameishaanza kuzoea kutumia mashine hizo. Katika kituo cha Majani ya
Chai, Uwanja wa Ndege alisema hali ni ngumu na mashine zinasumbua kiasi
ambacho watu walianza kufanya fujo mpaka askari Polisi walipoingilia
kati.
Inaelezwa juzi waliandikisha watu 105,
lakini jana, ikiwa ni siku ya pili ya uandikishaji, kufikia mchana
waliandikishwa watu 29 tu. Temeke walia na mashine Nako katika Manispaa
ya Temeke, watu waliendelea kumiminika vituo vya kuandikisha kupigakura,
lakini wengi walijikuta wakikwama katika foleni ndefu, sababu kubwa
ikielezwa ni changamoto za mashine pamoja na utaalamu mdogo wa matumizi
ya kompyuta.
Mkazi wa Temeke Wailes, Moses Felix
alisema hayo alipokuwa akizungumza na HabariLeo kuhusiana na
uandikishwaji huo unavyoendelea. “Waliokuja kujiandikisha ni wengi,
lakini wanaoondoka ambao tayari wamehudumiwa ni wachache hawazidi 30,”
alisema Felix.
Mjumbe wa Shina ambaye ni wakala wa CCM
katika uandikishwaji huo katika eneo la Miburani, Steven Mkundi alisema
changamoto iliyopo ni kukatika kwa ‘network’ kwa mashine hizo.
“Mashine
zilizopo mara nyingi network haifanyi kazi inachukua muda mrefu sana
huku msururu ukiwa ni mkubwa. Lakini katika eneo hilo wananchi
wamejitokeza kwa wingi, wamehamasika,” alisema.
Alisema juzi watu walioandikishwa katika eneo hilo walikuwa ni 95, hadi jana mchana tayari watu 67 walikuwa wameshajiandikisha.
Alisisitiza kuwa tatizo lingine
linalojitokeza ni kutokana na uchakavu wa mashine, pamoja na muda wa
kuanza kujiandikisha. Imeandikwa na Regina Kumba, Theopista Nsanzugwanko
na Lucy Ngowi
HABARILEO
Ziara ya kihistoria ya Rais wa Marekani, Barack Obama
nchini Kenya inatarajiwa kusimamisha shughuli nchini kwa muda kupisha
ujio wa kiongozi huyo wa taifa kubwa, lenye nguvu za kijeshi, kisiasa na
kiuchumi duniani.
Miongoni mwa shughuli zitakazosimama ni
usafirishaji wa anga, kwani mamlaka inayosimamia safari za ndege nchini
Kenya (KCAA), imetangaza kuwa anga la Kenya leo litafungwa kwa dakika
hamsini ili kuruhusu ndege ya Obama kutua katika Uwanja wa Ndege wa
Kimataifa wa Jomo Kenyatta, Nairobi.
Kwa mujibu wa shirika hilo, agizo hilo
litatekelezwa katika viwanja vyote vya ndege vya Kenya na kuwa anga hiyo
itafunguliwa baada ya ndege hiyo ya Rais Obama itakapokuwa imetua.
Shirika hilo limeyaandikia mashirika
yote ya ndege na pia kampuni zote za usafiri kuhusiana na agizo hilo na
kuwa safari za ndege kadhaa zitacheleweshwa leo na Jumapili, ambapo
zitachelewa kwa dakika 40 wakati Rais Obama atakapokuwa akiondoka Kenya
kwenda Addis Ababa, Ethiopia.
Awali, Idara ya Polisi nchini Kenya
ilikuwa imetangaza kuwa anga lote la Kenya lingefungwa siku tatu kabla
ya ziara hiyo. Lakini, kwa mujibu wa KCAA ndege zote zinazopaa chini ya
futi 20,000, hazitaruhusiwa kutua katika uwanja wa Jomo Kenyatta na ule
wa Wilson mjini Nairobi leo hadi Jumatatu.
Agizo hilo sasa linamaanisha ndege zote
ndogo, ambazo huhudumu kati ya Nairobi na Somalia na viwanja vingine
vidogo katika kanda ya Afrika Mashariki, hazitaruhusiwa kutua Nairobi
hadi mkutano wa kimataifa wa kibiashara ambao Obama atahudhuria
utakapomalizika.
Obama anatarajiwa mjini Nairobi siku ya
Ijumaa usiku, ambapo anatarajiwa kuwa mwenyeji wa kongamano hilo la
kibiashara pamoja na mwenyeji wake, Rais Uhuru Kenyatta. `Marufuku’ hiyo
inagusa pia baadhi ya barabara muhimu za Jiji la Nairobi, ambazo
zitafungwa kupisha ugeni mzito wa Obama ambaye anatua Kenya kwa mara ya
kwanza akiwa Rais wa Marekani, licha ya ukweli kwamba ana asili ya nchi
hiyo ya Afrika Mashariki.
Baba wa Rais Obama, Dk Hussein Obama
ambaye kwa sasa ni marehemu, ni mwenyeji wa kijiji cha Kogelo ambako
rais huyo wa Marekani, amewahi kutembelea kuona ndugu zake kwa upande wa
baba.
Licha ya Ubalozi wa Marekani kutangaza
kuwa Rais Barack Obama hakusudii kutembelea kijijini Kogelo, Magharibi
mwa Kenya, bado matarajio ni makubwa miongoni mwa wakazi wa eneo hilo.
Kogelo, kijiji ambacho hakikujulikana hata nchini Kenya zaidi ya miaka
kumi iliyopita, hivi sasa kinatajwa katika magazeti, redio na
televisheni kote duniani, kama nyumbani kwa baba yake Rais Barack Obama,
Barack Hussein Obama Senior.
Makaburi ya babu yake Rais Obama,
Hussein Onyango Obama na Barack Obama Senior, yamewekwa vigae vipya na
tayari kokoto zimemwagwa pembeni kuzuia vumbi iwapo wageni watakuja.
Aidha, makazi ya Mama Sarah Obama, bibi
wa Rais Obama yamekuwa yakiboreshwa zaidi, huku wakazi wa kijiji hicho
wakihoji sababu za kupuuzwa na serikali ya Marekani, wakidai Obama
alistahili kwenda kusalimia ndugu zake.
Hata hivyo, Mama Sarah amedai kuwa
alipokutana na Rais Obama Novemba mwaka jana huko Marekani, alimweleza
angekuja kuzuru kaburi la baba yake. “Lazima atafika hapa kuona kaburi
la baba yake,” alisema Mama Sarah Obama.
HABARILEO
Aliyekuwa mwanachama mashuhuri na mbunge wa miaka mingi kwa tiketi ya CUF, Hamad Rashid ametangaza kukiacha chama hicho na kuhamia chama cha Alliance for Democratic Change (ADC).
Ameahidi kuwa atawania urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, endapo chama chake hicho kipya kitamthibitisha.
Aidha, ameelezea kufurahishwa kwa
mapokezi aliyoyapata na kuongeza kuwa anashauri vyama vya siasa vya
upinzani nchini, vibadilishe mitazamo ili viwe taasisi na kupokezana
vijiti kwenye nyadhifa za uongozi.
Rashid aliyasema hayo jana Dar es
Salaam, wakati wa mkutano wa chama hicho wa kupokea wanachama wapya,
waliojiunga na ADC, akiwemo yeye, ambaye alipewa kadi namba moja ya
chama hicho na kurudisha kadi ya CUF.
Rashid alisema umefika wakati sasa wa
vyama vya siasa vya upinzani kubadilisha mtazamo na kuwa taasisi badala
ya kuonekana ni chama kinachoongozwa na mtu mmoja, kwani jambo hilo
halileti demokrasia wala haki.
“ADC
msirudie dhambi ya vyama vingine vya upinzani, tuwe na ukomo wa
madaraka na chama kiwe taasisi ambayo uongozi ni kupokezana vijiti, hii
ndiyo haki ni moja ya jambo lililonivutia kujiunga na ADC, kuna ukomo wa
madaraka, sio zaidi ya miaka 10”, Rashid.
Alisema chama kisichojenga makada wa
kurithi ni chama chenye matatizo ya uongozi na kwamba chama ili
kiendelee ni lazima kijenge watu watakaorithi baada ya ukomo wa nyadhifa
zao kufika na kukitaka ADC, kuhakikisha kinajijenga kuwa taasisi ili
kiendelee.
Akizungumzia shutuma zinazotolewa dhidi
yake kuwa yeye ni msaliti, alisema hajawahi kuwa msaliti, bali
ataendelea kuwa mkweli hata kama ukweli huo unauma. “Nimeitwa
msaliti, ila nakumbuka mwaka 1988 nilifukuzwa CCM, nilisema ukweli na
hata nilipokuwa CUF, nilisema chama hakiendi kwa sababu kinaongozwa kama
mtu binafsi na sio taasisi, na mabilioni ya fedha yaliliwa, sasa huo
ndio usaliti?” Rashid.
Aliwataka ADC na wanachama wake,
kutomkasirikia mwanachama yeyote atakayeamua kwa ridhaa yake kuhamia
chama kingine, kwani ana haki ya kufanya hivyo na kamwe wasiwaone ni
maadui.
Akizungumzia mwelekeo wa siasa nchini,
Rashid alisema hivi sasa siasa za Tanzania zimebadilika sana na kuwa
siasa za fedha na kwamba ni vyema wananchi wakamuogopa Mungu, na kamwe
wasikubali kuhadaiwa na fedha , ili kuchagua viongozi.
“Siasa
za Tanzania zimebadilika, zimekuwa siasa za fedha, tafadhalini,
msikubali kudanganywa na wagombea wanaotoa fedha, huo sio uadilifu,
nilijifunza mambo matatu kwa Hayati Mwalimu Nyerere, uadilifu, kusimamia
maamuzi na kuwa karibu na watu, hivi ndivyo vitu vya msingi kwa
kiongozi na sio fedha”,Rashid.
Awali, Mwenyekiti wa Chama hicho, Said Miraji
alisema chama kitasimamisha wagombea katika uchaguzi ujao kwenye nafasi
mbalimbali kuanzia ya urais hadi madiwani, na kuwataka wanachama wake
hususan wanawake kujitokeza kuwania nyadhifa hizo.
NIPASHE
Watu kumi wamekufa kwenye ajali ya basi
la Simiyu lenye namba za usajili T.318 ABM iliyotokea juzi maeneo ya
Chalinze wilayani Chamwino mkoani hapa huku majeruhi na mashuhuda
wakisema chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi wa dereva.
Basi hilo ambalo lilikuwa likitokea Mwanza kuelekea Dar es Salaam ilitokea juzi saa 12:30 jioni. Baadhi ya majeruhi hao ambao walisema ajali hiyo ilitokana na mwendo kasi wa dereva. Mmoja wa majeruhi hao, Sawika Saganda (40), alisema watu wengi waliumia na kufa kutokana na kubanwa na viti.
Aidha, alisema wakati gari likiwa kwenye mwendo mkali tairi lilipasuka na ndipo gari lilisererekea msituni na kugonga mbuyu. Kwa upande wa mashuhuda wa ajali hiyo,
walisema ajali hiyo ilitokana na mwendo kasi wa dereva uliyochangia kwa
kiasi kikubwa gari kupoteza muelekeo na kuingia porini na kugonga mti.
Lucy Kalulu alisema chanzo kikubwa cha ajali hiyo kilisababishwa na mwendo kasi na ndiyo maana tairi likapasuka na gari kupoteza muelekeo.
Alisema gari lisingekuwa na mwendo kasi lingeyumba kidogo na kutulia bila ya kuingia msituni. Mganga Mkuu wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, Dk. Ezekiel Mpuya alithibitisha kupokea maiti nane na majeruhi 55.
Alisema maiti mbili ziliongezeka kutoka kwa majeruhi 55 ambao walikuwa kwenye matibabu.
Alisema waliokufa wakiwa hospitalini hapo ni mwanamke mjamzito, Rukia Mkupe na Mussa Kashinde.
Mbali na hao, wengine ni
Elias Mibawa, Mfungo Matutu, Emmanuel Binamungu, Salum Ramadhan,
Nestory Ambloz, Shimba Masungu, Maduhu Lushanga na Charles Mahushi.
NIPASHE
Shinikizo dhidi ya Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa,
la kumtaka akihame Chama Cha Mapinduzi (CCM) linazidi kuongezeka na
katika timu yake ya ndani ni watu wawili tu wanaonekana kumtaka abakie
ndani ya chama hicho.
Habari za ndani ya vikao vya kujadili
hatua za kuchukuliwa na Lowassa baada ya jina lake kukatwa kwenye
mchakato wa kugombea urais kupitia CCM, zinasema kuwa wandani wake
wanaamini kuwa hana atakachopata kama ataendelea kubaki kwenye chama
hicho tawala.
“Kaka
sikiliza, inavyoelekea shinikizo dhidi ya Lowassa ni kubwa sana. Watu
wake wa ndani wanataka aondoke CCM. Wanaona kama amedhalilishwa mno,” kilisema chanzo chetu ndani ya vikao hivyo.
Chanzo hicho kilichoomba kutokutajwa
jina kwa sasa, kilisema kuwa watu wake wa ndani wanaamini Lowassa
akiendelea kubaki CCM atakuwa amewavunja moyo wale wote waliompigania,
hasa vijana waliojaa matumaini ya kumuona akiongoza taifa hili.
Wandani wa Lowassa wanaamini kuwa kama
akiamua kujiunga na chama chenye nguvu cha upinzani anaweza kutimiza
ndoto yake ya kuwatumikia Watanzania kama rais wa awamu ya tano.
Chanzo chetu kinasema kuwa Lowassa
mwenyewe amekwisha kuamua kufanya uamuzi mgumu, ila kuna msuguano juu ya
namna ya kuondoka CCM.
Taarifa zaidi zinasema kuwa watu wawili katika timu ya ndani ya Lowassa ndio wanaelekea kuwa na mawazo tofauti. Hawa ni Rostam Aziz,
mwanasiasa na mfanyabiashara mashuhuri nchini na mtu mwingine
anayetofautiana na mkakati huu mpya wa kung’oka CCM ni mkewe, Mama Regina Lowassa.
Chanzo chetu kinasema kuwa wawili hao
wanaamini mapigo ambayo Lowassa amekumbana nayo ni mengi na yanatosha,
kwa maana hiyo ingefaa tu apumzike.
“Sijui
ni kwa nini RA (Rostam Aziz) anakuwa skeptical (shaka). Si unakumbuka
ndiye aliyesema amechoshwa na siasa uchwara… sasa sijui kwa nini
anapunguza makali,” chanzo kilisema.
Hata hivyo, vyanzo vyetu vinaongeza kuwa
pamoja na upinzani huo Lowassa anadaiwa kuwa amekwisha kuamua na
kinachosubiriwa sasa ni muda tu wa kutamka anakokwenda.
Wakati hali ikiwa hivyo ndani ya kambi
ya Lowassa, kuna taarifa za kuaminika kuwa kumekuwa na mashauriano baina
ya watu wake na viongozi waandamizi wa kambi ya upinzani juu ya
mwelekeo wake wa kisiasa.
Mwandani mwingine katika kambi ya
Lowassa alisema kimsingi yeye (Lowassa) amekwisha kuamua, anachofanya ni
kuona kwamba watu wake wa karibu hawadhuriki na uamuzi wake huo.Takriban wiki mbili sasa, Lowassa amekuwa na jambo kubwa moyoni analitaka kuwaambia Watanzania.